Home Blog

Mimea Dawa na Misitu Ilivyo Muhimu kwa Maisha ya Sasa na Baadaye

0

Siku ya wanyamapori duniani inatukumbusha kutafakari namna tunavyoishi na mazingira yanayotuzunguka. Mazingira kama misitu, miti, maji, hali ya hewa, wanyama na wadudu.

Hivyo siku ya wanyamapori duniani inatupa nafasi kutafakari njia na juhudi tunazofanya kwenye uhifadhi wa Maliasili zetu za wanyama na mimea kama zinatosha. Ni muhimu sana kujifanyia tafakari za kina kwasababu matokeo na takwimu zinaongea mengi kuhusu juhudi zetu kwenye uhifadhi wa Maliasili hizi muhimu.

Katika maadhimisho haya ya siku ya wanyamapori duniani, ambayo hufanyika kila mwaka tarehe 3 Machi, yana kuli mbiu mbali mbali. Kauli mbiu ya mwaka 2026, ni Mimea dawa na Manukato; Kuhifadhi Afya, Urithi na Maisha (Medicinal and Aromatic Plants: Conserving Health, Heritage and Livelihoods).

Mimea ni sehemu muhimu sana ya uhifadhi wa mazingira asilia ya wanyama na viumbe hai wengine. Mimea inahifadhi mamilioni ya viumbe hai wanaaonekana kwa macho na wasioonekana kwa macho. Mimea ndio huunda misitu, misitu ni mchanganyiko wa mimea ya aina nyingi inayoota sehemu fulani.

Picha ya misitu iliyopo Magharibi mwa Tanzania, Mkoa wa Kagera, picha na Hillary Mrosso

Mimea ina faida nyingi sana kama chanzo cha kuzalisha hewa ya oksijeni, makazi ya viumbe hai, kuhifadhi vyanzo vya maji, kuzuia mmomonyoko wa udongo, kudhibiti mabadiliko ya tabia nchi, vyanzo vya dawa za asili za binadamu na wanyama, malighafi za ujenzi na utalii.

Kwa kuzingatia kauli mbiu ya mwaka huu, mimea dawa na manukato; kuhifadhi afya, urithi na maisha. Mimea imekuwa sehemu muhimu sana kama chanzo cha dawa nyingi asilia, mimea imetumika sehemu nyingi kama manukato, mimea ni urithi wetu na maisha yetu.

Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonyesha kuwa, asilimia zaidi ya 80 ya watu duniani hutegema memea kama dawa. Lakini asilimia 25 ya dawa za kisasa zimetengenezwa kwa kutumia mimea. Hii inaonyesha jinsi mimea ilivyo sehemu muhimu ya afya ya mwanadamu.

Mimea mingi ambayo hutumika kama dawa na manukato hutokana na miti asilia. Kama iliyoripotiwa na Shirika la Chakula Duniani FAO kuwa, asilimia 60 hadi 80 ya mimea dawa yote hutoka katika miti au misitu asilia. Hii inatupa kufahamu kuwa misitu asilia ndio chanzo kikuu cha mimea na miti yote ambayo hutumiwa sehemu mbali mbali duniani kama dawa na manukato.

Kupitia taarifa hizo tunajifunza kuwa uhifadhi na utunzaji wa misitu yetu sio tu kama sehemu ya uhifadhi wa makazi ya wanyamapori, au hifadhi ya vyanzo vya maji, bali ni muhimu kwa uhifadhi wa vyanzo muhimu vya dawa kwa ajili ya afya na maisha ya binadamu.

Utafiti kutoka Chuo Kikuu cha Nelson Mandela nchini Tanzania umebaini kuwa, asilimia 80- 90 ya dawa zinazotengenezwa na kutumiwa na waganga wa jadi kwa ajili ya kutibu maradhi mbali mbali ya watu hupatikana kutoka katika miti asilia au misitu asilia.

Taarifa hii inaongeza uzito kwenye matumizi makubwa ya mimea asilia kama dawa, lakini pia inaonyesha picha nyingine kubwa kuwa mimea asilia inaweza kuvunwa au kukatwa bila kibali, hivyo kupelekea kuendelea kupotea na kutoweka bila taarifa za kutosha.

Hata hivyo, hapa tunaona upande mmoja wa uvunaji na matumizi makubwa ya mimea asili kama dawa. Bado kuna matumizi mengine mengi ya mimea asili kama mapambo, manukato, mbao, kuni, mkaa nk. Ambayo ni matumizi makubwa, hali hii inachangia sana mimea mingi kupotea bila kuwa na taarifa za kina.

Kuna ushahidi mwingine kutoka Shirika la TRAFFIC kuwa, asilimia 60 mpaka 90 ya mimea dawa na ya manukato iliyopo katika masoko na biashara imetoka katika misitu asilia. Utafiti huu uliofanywa na TRAFFIC unatuonyesha picha kubwa zaidi, huenda kuna biashara haramu nyingi za mimea asili kwa matumizi mbali mbali sehemu nyingi duniani.

Aina mbali mbali za mimea dawa inayozalishwa Tanzania Picha na y Julius Maricha & Herieth Makwetta kutoka The Citizine

Idadi kubwa ya mimea asili kuendelea kutumiwa kwa kiasi kikubwa kama dawa na mapambo sehemu mbali mbali duniani, imesababisha baadhi ya spishi au aina za mimea hii kuwa hatarini kutoweka kabisa mwituni.

Mimea mingi ya dawa iko hatarini kutoweka nchini Tanzania na kote ulimwenguni kutokana na uvunaji usio endelevu, hasa wa mizizi na magome. Hapa kuna mifano ya mimea ya dawa inayokabiliwa na hatari hiyo:

  1. Mkunungu (Zanthoxylum chalybeum): Unajulikana pia kama Oloisuki kwa Kimasai. Mmea huu unavunwa kwa kiasi kikubwa kwa ajili ya kutibu matatizo ya mfumo wa upumuaji, malaria, na maumivu ya tumbo.
  2. Mvumo wa Milimani (Warburgia salutaris): Mti huu unathaminiwa sana kwa kutibu maambukizi ya fangasi na bakteria, lakini idadi yake imepungua sana kutokana na uvunaji wa magome.
  3. Mpingo (Dalbergia melanoxylon): Ingawa unajulikana zaidi kwa mbao, pia una matumizi ya kidawa na unakabiliwa na hatari kubwa ya kutoweka kutokana na ukataji holela.
  4. Mninga (Pterocarpus angolensis): Hutumika kutibu magonjwa kama kuhara na matatizo ya ngozi, lakini unakatwa kwa wingi kwa ajili ya mbao na dawa.
  5. Mvule (Milicia excelsa): Mti huu mkubwa unatajwa kuwa miongoni mwa spishi zinazohitaji uhifadhi wa haraka nchini Tanzania kutokana na matumizi yaliyopitiliza.
  6. Mlonge (Moringa oleifera): Pamoja na kuwa unalimwa maeneo mengi, spishi za porini za jamii hii zinapotea kutokana na uharibifu wa makazi na uvunaji wa mizizi.
  7. Mti-sumu (Securidaca longipedunculata): Unatumika kutibu magonjwa mengi ya mfumo wa neva na ngozi, lakini ni miongoni mwa miti inayotoweka kwa kasi katika maeneo kama Shinyanga.
  8. Mvumbasi (Ocimum suave): Mmea huu unaonukia vizuri unavunwa sana kwa ajili ya kutibu mafua na matatizo ya tumbo, na hivyo kupungua katika maeneo ya Milima ya Tao la Mashariki.
Pichani ni Noah Salonick, mtaalamu wa tiba mitishaba akionyesha namna ya kuchanganya aina mbali mbali za mimea dawa jijini Dar es Salaam, Tanzania (Picha na Focus Faustine/WildAid)

Hiyo ni picha ya mimea ambayo kwasababu ya matumizi yake kuwa makubwa inaelekea kutoweka duniani. Pamoja na hayo, dunia inaendelea kupoteza maelfu na mamilioni ya hekari za misitu muhimu kutokana na sababu nyingine kama vile kilimo, kuchoma moto hovyo na kuongezeka kwa idadi ya watu.

Takwimu za dunia mwaka 2024, zinaonyesha dunia inakadiriwa kupoteza zaidi ya hekari milioni 8 za misitu asili. Na misitu hii ndio hubeba uhai wa viumbe wote duniani, inapotea kwa kasi kubwa sana.

Kuendelea kupotea kwa idadi kubwa ya misitu hii kunaendana sambamba na kuendelea kupotea kwa viumbe hai wengine ambao hutegemea misitu hii kama sehemu ya makazi, chakula na mazalia.

Asilimia 80 ya misitu hupotea kwasababu za maendeleo ya kilimo ambacho kinahitaji maeneo mapya na upanuzi wa mashamba, hata hivyo kuchoma moto misitu imekuwa ni moja ya changamoto kubwa iliyoongoza kwa mwaka 2024 kama kichocheo kikuu cha kupotea kwa misitu sehemu nyingi duniani.

Barani Afrika, misitu inapotea kwa kasi kubwa, inaripotiwa kuwa nusu ya upotevu wa misitu yote duniani hutokea barani Afrika. Mwaka 2015 hadi 2025, Afrika imepoteza zaidi ya hekari milioni 29.9 za misitu asilia. Kiasi hiki ni kikubwa sana ukilinganisha na upotevu uliotokea miongo kadhaa iliyopita.

Hata hivyo, inakadiriwa kuwa kiasi cha misitu inayopotea barani Afrika kila mwaka ni hekari milioni 3.45. Hii ni ishara mbaya kwa uhifadhi wa misitu asilia, idadi hii ni kubwa na inaendelea kuongezeka kila siku. Tunatakiwa kujiuliza, kasi hii ya upoteaji wa misitu inaendana na kasi ya uwekezaji katika uhifadhi wa misitu hii?

Kwa upande mwingine, Tanzania inashika nafasi ya 2 Kusini mwa Jangwa la Sahara na nafasi ya 3 duniani, kama nchi ambayo inaongoza kwa uharibifu na upotevu wa misitu yake asilia. Takwimu za mwaka 2024 pekee zinaonyesha Tanzania imepoteza zaidi ya hekari 469,000 za misitu yake asili.

Sababu za Tanzania kupoteza kiasi kikubwa hivi cha misitu yake ni pamoja na kilimo biashara, ambacho kimechangia asilimia 89 kwa ukataji miti, kilimo cha kuhama hama, mahitaji makubwa ya kuni, mkaa, kulisha mifugo eneo la hifadhi, majanga ya moto, ukataji mbao na miti kwa ajili ya ujenzi.

Picha hii inaonyesha namna misitu asili inavyovunwa kwa shughuli mbali mbali za kibinadamu kama vile kilimo, mkaa, kuni ujenzi, Picha na Hillary Mrosso.

Nchi nyingine zinazoongoza kupoteza misitu yake ni Brazili, ambayo inashika nafasi ya kwanza duniani kwa kupoteza hekari 2,942,000 za misitu kwa mwaka, ikifuatiwa na Angola ambayo inakadiriwa kupoteza hakari 510,000 za misitu yake asilia, nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo inafuata kwa kupoteza hekari 283,000 na Zimbabwe inashika nafasi ya nne kwa kupoteza hekari 267,000 ya misitu yake asilia kwa mwaka kama ilivyoonyeshwa hapa.

Ushahidi mwingine kutoka katika shirika la chakula duniani FAO unaonyesha nchi za ukanda wa Mashariki na Kusuni mwa Jangwa la Sahara zinakadiriwa kupoteza zaidi ya asilimia 53 ya maeneo ya misitu asilia katika bara la Afrika.

Kuendelea kupotea kwa misitu asilia kwa kasi kubwa hivi kunachochea majanga mengi kama vile mvua nyingi kupita kiasi, mafuriko, umasikini, ukame, njaa na magonjwa. Utunzaji wa misitu ni utunzaji wa afya na maisha yetu. Tutunze misitu hii kwa nguvu zetu zote.

Nchini Tanzania, asilimia zaidi ya 60 ya watu wanaishi vijijini, ambako ndio kwenye hifadhi ya misitu. Watu hawa wanahitaji matibabu, maji, kuni, mkaa, na huduma nyingine kutoka kwenye misitu ya karibu. Hivyo hutegemea misitu hiyo kwa mahitaji hayo na mengine.

Kuendelea kupotea kwa misitu hii kunapelekea kupotea kwa fursa za utalii na fura nyingine za uwekezaji kwenye misitu, kama vile miradi ya hewa ukaa. Miradi ya hewa ukaa hufanyika sehemu ambazo zina misitu iliyohifadhiwa vizuri kwa muda mrefu. Miradi hii imeleta na inaendelea kuleta fedha nyingi kwa serikali na jamii zenye misitu hii.

Wito wangu kwa jamii, tunatakiwa kutunza misitu, tusichome moto misitu yetu, ni muhimu sana kuliko tunavyofikiri. Fikiria ni miaka mingapi imepita hadi miti hiyo na misitu hiyo kufikia hapo ilipofikia. Utagundua ni miaka mingi sana, ukuaji wa misitu ni taratibu sana, lakini upotevu wake ni wa haraka sana.

Kitendo cha kukata miti na misitu iliyotumia zaidi ya mika 10-100 kufikia ilipo ni gharama kubwa sana. Huwezi kulinganisha na uhitaji na matumizi tunayotaka kufanya.

Tujihusishe kwenye kupanda miti mbadala, badala ya kuingia msituni kukata miti kwa ajili ya dawa, ni vizuri kutafuta namna ya kupanda miti hiyo kwenye maeneo yetu ili ikikua itumike kwa matumizi ya dawa, kuni, mapambo, ujenzi nk.

Tujitokeze kwenye program za kupanda miti, kusaidi kurudisha miti iliyopotea.

Kwa afya bora na maisha mazuri kwa viumbe wote, tutunze mimea na misitu yetu!


Imeandikwa na Hillary Mrossso
+255 683 864 2481
Email: hmconserve@gmail.com

Safari ya Hillary Thomas Mrosso Katika Uhifadhi wa Wanyamapori Tanzania

0

Wakati nasoma elimu ya msingi na sekondari, nilikuwa na ndoto za kuwa daktari wa binadamu, hivyo nilipenda sana masomo ya sayansi, na pia nilikuwa naweza kufanya vizuri ili nijie kutimiza ndoto yangu ya kuwa daktari hapo baadaye.


Lakini siku moja wakati wa likizo nikiwa nyumbani, nilikutana na mzee mmoja amestaafu, aliyewahi kufanya kazi katika hifadhi za taifa Tanzania, maarufu kama TANAPA. Huyu mzee nilikutana naye hapo nyumbani kwake akiwa kibarazani anasoma magazeti maarufu yaliyoitwa KAKAKUONA.


Magazeti haya yalikuwa yanaelezea uzuri wa hifadhi za taifa, wanyamapori, na Maliasili zinazopatikana Tanzania, magazeti haya yalipambwa na picha nzuri zenye mvuto kuhusu wanyama na tabia zao, mambo ya kipekee ya wanyamapori na uoto asilia. Siku hizi haya magazeti hayapo tena.


Niliongea na yule mzee mambo mengi kuhusu wanyamapori, hifadhi za taifa na utalii. Baadaye nilimuomba baadhi ya magazeti hayo ili nikajisomee nyumbani, yule mzee alinipa magazeti kama 5 hivi. Nilipofika nyumbani nilianza kuyasoma yote. Kwa kweli nilivutiwa sana na hadithi nzuri za wanyama na maisha yao, hifadhi za wanyamapori na mandhari nzuri za wanyama nchini Tanzania.


Tangu siku ile niliamua kubadili kabisa ndoto yangu ya kuwa daktari wa binadamu na kutaka kusomea mambo ya uhifadhi wa wanyamapori. Baada ya kumaliza kidato cha sita, nilichagua kusomea Shahada ya Usimamizi wa Wanyamapori katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine.
Nilifurahia sana masomo na mafunzo kwa vitendo, hasa tulipokuwa tunaenda hifadhini kwa ajili ya elimu ya mafunzo kwa vitendo, kama vile kujua tabia za wanyama, njia zinazotumika kuhesabu wanyamapori wakubwa kwa wadogo, njia zinazotumika kuhesabu ndege na kuwatambua na namna ya kupima uoto wa asili.


Nilikuwa nafurahia sana maana huku tunaona wanyama wengi wakiwa katika mazingira yao, tuliwaona tembo, nyati, fisi, simba, twiga, nyani, ngiri, nyumbu, pundamilia, swala na ndege wa aina nyingi. Tulifundishwa mbinu nyingi za uhifadhi wa wanyamapori na changamoto zake kama vile ujangili, uchomaji moto, mimea vamizi, na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi.


Baada ya kumaliza shahada ya kwanza katika uhifadhi wa wanyamapori, niliendelea kujifunza kupitia makala mbali mbali za wanyamapori na uhifadhi, nilikuwa nasoma majarida ya kisayansi kuhusu wanyamapori na uhifadhi na kufuatilia habari za wanyamapori.


Hata hivyo, nilibahatika kupata nafasi ya kujitolea katika mradi wa Kanivora ambao unafanya kazi zake katika eneo la Ruaha, Iringa Tanzania. Nilifurahi sana kupata nafasi hii ya kujitolea ili kujifunza kwa undani na kwa vitendo namna jamii zinavyoishi na wanyamapori, hasa kanivora. (kanivora ni wanyama wanaokula nyama, kama simba, chui, mbwa mwitu, fisi, duma nk). Baadaye niliajiriwa na mradi huu kama mtafiti msaidizi.


Nikiwa katika mradi huu wa kanivora ndio niliona mambo yalivyo halisi, changamoto, na faida za kuishi na wanyamapori. Niliona jinsi kanivora wakubwa kama simba, chui na fisi walivyokuwa wanasababisha migogoro kwa wafugaji, walikuwa wanakula mifugo na kuleta migogoro isiyoisha. Pamoja na hayo, eneo hili la Ruaha lina changamoto nyingi za wanyamapori kama tembo, nyani na ndege, wanakula mazao na kuharibu mali za watu.


Hata hivyo nikiwa katika mradi wa kanivora, tulitumia njia mbali mbali kupunguza migogoro hiyo kama vile kuwajengea mazizi imara ya waya, ambapo simba na fisi hawawezi kuingia na kula mifugo. Mimi nilikuwa nasimamia programu za vijiini, kuelimisha watu na jamii kuhusu kanivora, lakini pia nilisimamia programu ya utoaji wa faida zinazotokana na uwepo wa wanyamapori kwenye maeneo ya vijiji katika eneo la Ruaha. Mradi wa kanivora unatoa hela nyingi sana kwa jamii zinazoishi kando ya hifadhi ya Ruaha ili kusaidia jamii kuvumilia kuishi na kuhifadhi kanivora.


Mwaka 2017, ndio nilipata wazo la kuanzisha blogu hii ya WILDLIFE TANZANIA kwa ajili ya kushirikisha jamii kubwa zaidi mambo ya uhifadhi wa wanyamapori, faida zake na changamoto zilizopo katika uhifadhi kwa ujumla. Hii ilinisaidia kuandika baadhi ya makala na hadithi kuhusu uhifadhi, faida zake na changamoto zake, hadi sasa bado naenelea na kuandika makala hizi.


Tumeandika zaidi ya makala 400, kwenye maeneo mbali mbali kama uhifadhi, ujangili, biashara haramu za wanyamapori na utalii. Hata hivyo, nimewasaidia wengine pia zaidi ya 15 kuandika makala nzuri zenye kutoa elimu kwa jamii kuhusu uhifadhi.


Mwaka 2019, niliacha kazi katika mradi wa kanivora kwa lengo la kujiendeleza zaidi kwa elimu ya uzamili, (masters), ambapo nilimaliza mwaka 2021. Elimu hii imekuwa chachu ya kukuza sana uelewa wangu kuhusu uhifadhi na kuona mambo kwa undani zaidi.
Disemba 2021, mimi na wenzangu tulianzisha taasisi ya utafiti na uhifadhi Tanzania. Lengo likiwa kuwa sehemu ya suluhisho kwa changamoto zilizopo katika uhifadhi. Katika taasisi hii tunafanya tafiti nyingi za kakakuona, tembo na twiga. Tulitumia uzoefu tuliopata kwenye miradi na taasisi nyingine tukanzisha taasisi hii.


Pamoja na mambo mengine tumekijita kutafiti zaidi kakakuona, wanyama ambao wapo hatarini kutoweka, lakini hakuna taarifa za kutosha kuhusu wanyama hawa hapa Tanzania, hata uelewa wa jamii kuhusu wanyama hawa ni mdogo sana. Lakini kakauona ni wanyama walio hatarini kutoweka kutokana na biashara haramu, kupungua na kuharibika kwa makazi yao, ukosefu wa tafiti, imani potofu kuhusu kakakuona na ukosefu wa uelewa kuhusu wanyama hawa.


Hadi sasa machapisho mawili ya kisayansi kuhusu kakakuona yameshatoka. Mengine 5 yapo katika hatua za mwishoni kutoka. Hii imesaidia kutoa taarifa za kina kuhusu wanyama hawa na mitazamo ya watu kuhusu wanyama hawa wa kipekee.


Juhudi hizi na nyingine katika uhifadhi, zimefanya nichaguliwe na Wizara ya Maliasili na Utalii kuwania tuzo za Mshawishi Bora katika masuala ya Uhifadhi (Best Conservation Influencer). Nawashukuru sana wale walionipigia kura ili nishinde tuzo hii, pia wale waliojitoa kuwashirikisha wengine ili nipate kura kwa ajili ya tuzo hii muhimu.


Tuzo hii itakuwa chachu kubwa sana katika safari yangu ya uhifadhi, pia inaonyesha mchango wetu katika uhifadhi unaonekana na kudhaminiwa. Hii inatia moyo na kufariji na kufariji sana.
Mwisho wa kupiga kura ni tarehe 27/01/2026. Kama bado hujapiga kura, tafadhali naomba unipigie kura kuwa Best Conservation Influencer.

Nitaweka hapa link na utaratibu wa kupiga kura.
Bonyeza link hiyo HAPA SERENGETI AWARD
Utaona sehemu imeandikwa, Search for Applicant,
• Hapo utaandika jina langu, Hillary Thomas Mrosso,
• Utaendelea chini, itakuletea kipengele cha besti conservation influencer na picha yangu utaona hapo
• Utabonyeza hapo, halafu chini utaona sehemu ya kuweka email au namba ya simu.
• Utaweka namba ya simu kuanzia na +255, utaweka namba yako ya simu au email yako
• Ukifanya hivyo utapokea ujumbe wa uthibitisho kuwa umepiga kura tayari, ya verification code.
• Hapo utakuwa umepiga kura tayari.

Ukipata changamoto yoyote tafadhali wasiliana na mimi kwa namba hizi
NICHAGUE TUENDELEE KUFANYA MAKUBWA KWENYE UHIFADHI.
+255 683862481
Hillary Mrosso.

Zijue Sababu za TAWIRI Kukataa Matokeo ya Utafiti wa Duporge na Wenzake Kuhusu Idadi ya Nyumbu Katika Eneo la Serengeti – Masai Mara, Tanzania

0

Uhifadhi endelevu wa wanyamapori unahitaji tafiti za kina za mara kwa mara kwa kutumia mbinu sahihi zilizohakikiwa ili kuleta matokeo halisi yanayosaidia katika kuweka mipango endelevu ya uhifadhi.

Tafiti ni mihimu sana katika uhifadhi wa wanyamapori. Lakini tafiti hizi zinatakiwa kufanyika kwa weledi mkubwa kwa kuzingatia mbinu au njia za kufanya utafiti zilizohakikiwa na kukubaliwa katika ulimwengu wa sayansi na tafiti.

Hata hivyo ni jambo la kawaida katika ulimwengu wa sayansi na tafiti, kukosoana, kupendekeza maoni au kutoa ushauri endapo mbinu mpya au njia nyingine ya utafiti imetumika na kuleta matokeo tofauti na njia za awali zilizowahi kutumika.

Mfano, matokeo ya utafiti wa hivi karibuni tarehe 9/09/2025, uliochapishwa katika jarida la PNAS Nexus kuhusu idadi ya nyumbu wanaopatikana katika mfumo wa ikolojia ya Serengeti Masai- Mara, umeonyesha idadi ya nyumbu katika eneo hilo ni 600,000 badala ya nyumbu zaidi ya milioni 1.3 kama ilivyoripotiwa na tafiti nyingi za awali.

Matokeo ya utafiti huo wa Isla Duporge na wenzake umezua taharuki, mshangao na maswali mengi kwa baadhi ya watafiti na wahifadhi wa wanyamapori sehemu mbali mbali duniani, ikiwemo Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakifanya tafiti za nyumbu katika eneo hilo.

Hata hivyo, TAWIRI hawakukaa kimya kuhusu matokeo ya chapisho hilo la Isla Duporge na wenzake, walitolea ufafanuzi wa kina kuhusu matokeo ya utafiti huo na kutokubaliana na namna ulivyofanyika, njia walizotumia nk.

Picha kutoka Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), 2023

Huu ndio ufafanuzi kutoka Taasisi ya Utafiti wa wanyamapori Tanzania (TAWIRI); karibu tuusome ili tufahamu sababu za kukataa matokeo ya chapisho hilo.

UFAFANUZI JUU YA CHAPISHO LA ISLA DUPORGE et al., 2025, KWENYE JARIDA LA PNAS NEXUS KUHUSU IDADI YA NYUMBU KATIKA MFUMO IKOLOJIA WA SERENGETI-MAASAI MARA

Taasisi imelipitia kwa kina chapicho la Isla Duporge na wenzake liliotolewa kwenye jarida la PNAS Nexus (Brief report; https://10.1093/pnasnexus/pgaf264, Advance press publication la tarehe 9 Septemba 2025 na kuja na maoni kama ifuatavyo.

Kwanza itoshe tu kusema kuwa matokeo ya idadi ya nyumbu yaliyotolewa (600,000) siyo sahihi ukilinganisha na idadi ya sensa ya TAWIRI ya nyumbu 1,366,109 (SE231,741) kwa  sababu ya mapungufu mengi ya kimethodolojia (methods) kwa maana ya namna (design/ approach) na mbinu (technique) ya namna aina hiyo mpya ya kuhesabu nyumbu (soroveya) ambayo ndio inafanyiwa majaribio na inayofanyika kwa mara ya kwanza kwa idadi kubwa ya wanyamapori kama nyumbu ilivyotekelezwa, ikilinganishwa na methodolojia ya kuhesabu nyumbu ambayo imehakikiwa na imekuwa ikitumika kwa muda mrefu na TAWIRI na pia nchi nyingine (Gold Standard method). Hivyo matokeo yake kamwe hayawezi kulinganishwa na idadi iliyotolewa na TAWIRI kwa miaka mingi.

Mapungufu yaliyobainika ambayo yanafanya idadi hiyo ya nyumbu kuwa siyo sahihi ni kama ifuatavyo;

Mbinu (census method) ya kuhesabu nyumbu inayotumiwa na TAWIRI ni ya kupiga picha kwa kamera za hali ya juu sana kwa kutumia ndege inayoruka kima kifupi [Aerial census, Aerial Point Sampling (APS)] ambayo imetumika kwa muda mrefu na imehakikiwa (validated), wakati mbinu iliyotumiwa na Duporge et al ni ya Akili mnemba/ bandia (Artificial Intelligence (AI) based survey, ya picha za satellite tu.

Njia hii ni mpya, haijahakikiwa (not validated), na ni mara ya kwanza inajaribiwa kuhesabu wanyamapori wengi kama nyumbu na katika mzingira tofauti, na haya ni matokeo yake ya kwanza kutolewa, ambayo yametofautiana sana na mbinu zilizohakikiwa, na yametoa idadi ndogo ya nyumbu ambayo haijawahi kutolewa na haina uhalisia.

TAWIRI hufanya sensa ya nyumbu kipindi cha masika (Februari-Machi), kipindi ambacho kundi zima limekusanyika kwenye maeneo ya mbuga za nyasi fupi (short grassland plains) wakati sensa ya Duporge et al imefanyika kipindi cha kiangazi (August 2022 na 2023) ambapo nyumbu wameshaondoka na wapo kwenye maeneo yenye miti na vichaka na kundi limeshatawanyika maeneo mapana.

Hivyo matokeo ya masika hayawezi kulinganishwa na matokeo ya kiangazi, maana nyumbu wanazunguka hasa kufuata chakula na maji, na huwezi kuwaona hata kutoka angani wakiwa ndani ya miti na vichaka.

TAWIRI hufanya Sensa kipindi ambacho nyumbu wako kwenye nyanda za nyasi fupi (southern Serengeti, northern Ngorongoro and Loliondo plains) ambako nyumbu ni rahisi kuonekana kwene picha zinazopigwa na kamera za ndege, wakati sensa ya Duporge et al imefanyika wakati nyumbu wakiwa wametawanyika katika uwanda wa miti au ‘woodlands’ (northern Serengeti and southern Maasai Mara) nchini Kenya, ambako ni vigumu kuwaona nyumbu wote kwenye picha za satellite kutokana na kufunikwa na miti (‘canopy inteference’), hali ambayo haiwezi kuleta idadi sahihi ya wanyamapori kwa aina zao.

Mbinu inayotumiwa na TAWIRI hutumia picha za kamera zenye uangavu au ‘resolution based on height’ wa 3-5cm ambazo zinauwezo mkubwa wa kuona/ kutambua na kutofautisha nyumbu, wakati Duporge et al ametumia picha za satellite za uangavu wa 33-60cm, ambazo zina uwezo mdogo wa kuona/ kutambua/ kutofautisha nyumbu na wanyamapori aina nyingine na hivyo kutowaona nyumbu wengi. ‘The TAWIRI 3-5cm high resolution images provide greater precision and counts than 33-60cm used by Durpoge et al.’

TAWIRI hufanya sensa ya nyumbu wengi wao wakiwa katika mfumo ikolojia wa Serengeti, na inahesabu upande wa Tanzania tu, wakati Duporge et al soroveya yake imejumuisha Tanzania na Kenya, kipindi ambacho nyumbu wametawanyika kotekote.

TAWIRI hufanya sensa zake wakati wa asubuhi, nyumbu wakiwa wako uwandani na wanakula, na hivyo nyumbu wengi kuonekana, wakati picha za satellite (satellite overpasses) zilizotumika na Duporge et al. zinapigwa mchana, kipindi ambacho nyumbu wengi wanakuwa wamepumzika chini ya miti na vichaka, na hivyo wengine kutoonekana.

Nje na muda wa soroveya au kuchukuliwa kwa picha, picha za satellite vilevile zinaathiriwa sana na mawingu, uoto, nk.

Mwisho, imeonekana kuwa tofauti ya idadi ya nyumbu aliyopata Duporge et al. imetokana na utofauti na uwezo mdogo wa mbinu waliyotumia ya satellite image kuona, kutambua na kuhesabu nyumbu, licha ya kuwa eneo linalotumiwa na TAWIRI kuhesabu nyumbu (kilometa za mraba 4,782) liko karibu sawa na eneo lililotumiwa na Durpoge et al. kwa soroveya yao. Na hivyo njia hiyo mpya na iliyotumika kwa mara ya kwanza kuhesabu nyumbu waliyotumia bado inahitaji utafiti wa kina na maboresho ya muda mrefu kabla ya kuamika na kutoa matokeo sahihi.

Tunahitimisha tena kuwa, matokeo haya ya idadi ya nyumbu (600,000) siyo sahihi kutokana na mapungufu mengi ya kiufundi ya soroveya hiyo ilivyofanyika kama yalivyoainishwa hapo juu. Kwa njia waliyotumia Duporge et al. hawangeweza kupata idadi halisi ya nyumbu. Hivyo matokeo yao hayawezi hata kidogo kutumika kulinganisha na idadi ya nyumbu iliyopatikana kwa kutumia ‘Gold standard method’ ya kuhesabu nyumbu.

Tunawashukuru wote kwa uvumilivu wenu. Wataalamu wa Taasisi na wadau wake wanaendelea kulifanyia kazi jambo hili. Imebidi kutumia maelezo marefu kufafanua maana jambo hili liweze kueleweka vizuri.

AHSANTENI SANA.

DKT. JULIUS D. KEYYU

DIRECTOR OF RESEARCH

SHAIRI: Tutunze Makazi ya Simba

0

Picha imepigwa na Hillary Mrosso, katika hifadhi ya Taifa ya Nyerere, Tanzania

1.Ndugu zangu karibuni, nina jambo kutamka
Simba wapo hatarini, majangili wawasaka
Waharibu masikani, kuvuka yao mipaka
Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

2.Simba waisha porini, hali sipobadilika
Hatua tuchukueni, tusije tukaumbuka
Wabaya tuwajueni, ikibidi kuwashika
Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

3.Mikakati tuwekeni, ujangili tumechoka
Mizaha tweke pembeni, na tuingiwe mashaka
Sijekuwa masikini, uchumi wetu kushuka
Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

4.Zaja hela za kigeni, Utalii kifanyika
Tutafuta na madeni, nchi itaheshimika
Tutatamba duniani, washindi tutaibuka
Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

5.Simba haba hifadhini, malaki hawajafika
Waweza usiamini, lakini waongezeka
Siweke silaha chini, bado hatujaridhika
Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

6.Kalamu naweka chini, nimechoka kuishika
Nimefikia mwishoni, wa shairi kuandika
Wekeni haya moyoni, daima kuyakumbuka
Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

Hillary Mrosso| mrossotm@gmail.com
+255 683 862 481 |Morogoro| 10.08.2025

Shairi: Agosti kumi ya Simba

1

Picha imepigwa na Sheridan Wright, katika hifadhi ya taifa ya Serengeti, Tanzania

Leo twendeni mbugani, utalii mbuga zetu
Huko leo kuna nini, nataka ninene kitu
Leo huko duniani, siku ya bingwa wa mwitu
Agosti kumi ya Simba, ni jukumu tuwatunze

Simba ni bingwa wa mwitu, hakuna asiyejua
Anaogopwa na watu, na mbio wakatimua
Mnyama ni mthubutu, mwendo wake wa hatua
Agosti kumi ya Simba, ni jukumu tuwalinde

Simba huyu maarufu, kivutio duniani
Ila twaingia hofu, wachache wasothamini
Ni watu waharibifu, wawawindao porini
Agosti kumi ya Simba, ni jukumu tuwatunze

Tudhibiti majangili, waletao maumivu
Tuwe na moja kauli, na pamoja zetu nguvu
Mbinu zote mbalimbali, dhidi ya wa nia ovu
Agosti kumi ya Simba, ni jukumu tuwalinde

Tusifunge yetu macho, kila mara tuwalinde
Hadi kizazi kijacho, watusifu watupende
Kuwa tulikuwa jicho, wasituponde ponde
Agosti kumi ya Simba, ni jukumu tuwatunze

Siku hii ya Simba, tulinde hii zawadi
Hata simba mwenye mimba, alindwe tena zaidi
Kutolinda ni kuchimba, shimo letu makusudi
Agosti kumi ya Simba, ni jukumu tuwatunze

Kuwatunza ni muhimu, kivutio cha wageni
Tuwalinde zamu zamu, pato lisishuke chini
Wakiwa hawa adimu, tutapotea sokoni
Agosti kumi ya Simba, ni jukumu tuwalinde

Malenga wa Ubena
+255 676 559 211
Uhifadhi
Wildlife Tanzania

Shairi: “Bundi ndege wa pekee ( U-1)

0

Karibu kwenye shairi linalohamasisha uhifadhi wa ndege aina ya Bundi. Shairi hili limendikwa na Dr. Raymondi Mgeni, maarufu kama Malenga wa Ubena, unaweza kusoma na kuwashirikisha wengine. Karibu!

Bundi aina ya Spotted-Eagle, anapatikana katika milima ya Usambara. Picha na Ezra Mremi

Zipo imani potofu, zimwandamazo bundi
Jamii hujawa hofu, navyo vitu haviendi
Bundi si mharibifu, kwanini hatumpendi ?
Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

Jamii imeamini, bundi kabeba mikosi
Wakimuona nyumbani, wanajawa wasiwasi
Wasema leo kunani, wataja hii nuksi
Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

Tena bundi akilia, hawazizimi taa
Hofu inawaingia, kuwa sasa ni balaa
Wanajua lawajia, tetesi zitazagaa
Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

Kahusishwa na uganga, na haramu biashara
Nia ovu wanapanga, bundi apate madhara
Avamiwa na mapanga, eti anatisha sura
Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

Bundi anazo faida, na nyingi za ikolojia
Si wa alama ya shida, wa kuleta mbaya njia
Ni ndege wa kawaida, na vingi husaidia
Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

Twaona zipo dalili, ndege kutupokonyoka
Spishi zake mbalimbali, kuja kesho kutoweka
Hili tulione mbali, na jamii ikazinduka
Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo

Tutoe hii elimu, jamii na kila kona
Ni biashara haramu, bundi kutafutwa sana
Uwepo wake muhimu, nayo kubwa tu maana
Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

Picha ya Bundi, imepigwa na Ezra Mremi

Malenga wa Ubena
+255 676 559 211
raymondpoet@gmail.com
Uhifadhi wa Bundi
Wildlife Tanzania

Yaliyojificha Nyuma ya Biashara Haramu na Matumizi Makubwa ya Ndege Bundi

0

Utangulizi

Katika misitu, mashamba na karibu na makazi ya watu, nyakati za usiku husikika sauti zisizo za kawaida.

Jua linapozama huamka ndege wawindaji ambao mara nyingi huonekana kama ishara ya jambo baya, na ndege hao ni bundi.

Lakini je, kweli bundi ni ishara ya kifo au ni viumbe muhimu wanaostahili heshima na ulinzi?

Makala hii inalenga kubainisha uhalisia wa maisha ya bundi, upekee wao wa kisayansi, changamoto wanazopitia kutokana na imani za kishirikina, na hitaji la haraka la kuwaelimisha watu juu ya umuhimu wa kuwalinda.

Upekee wa Bundi

Bundi ni ndege wa kipekee wanaofanya shughuli zao usiku, japo zipo jamii chache za bundi hufanya shughuli zao mchana.

Wana uwezo mkubwa wa kuona gizani, kusikia sauti kwa usahihi mkubwa, na kuruka kimya kimya bila kusikika kabisa.

Hii huwafanya kuwa wawindaji hodari wa panya, nyoka, ndege, popo, wadudu na viumbe wengine wadogo, hivyo kusaidia kulinda afya ya mazingira na mashamba ya watu.

Tanzania ni miongoni mwa nchi zenye aina za bundi ambao hawapatikani sehemu nyingine duniani kama bundi mtiti wa Sokoke (Otus ireneae) na bundi-tai wa Usambara (Bubo vosseleri). Soma hapa kufahau zaidi aina za bundi waliopo Tanzania

Hawa bundi ni wa pekee sana na wako hatarini kutoweka kutokana na changamoto mbalimbali zinazowakabili.

Licha ya umuhimu wao wa kisayansi, bundi wanakabiliwa na changamoto kubwa zinazotokana na uharibifu wa mazingira, imani potofu, mila zinazochochea matambiko, na biashara haramu.

Pichani kushoto ni Bundi-tai wa Usambara, na kulia ni Bundi mtiti wa Sokoke; Picha na Ezra Mremi

Mila na Imani Zinazohusishwa na Bundi Nchini Tanzania na Afrika Mashariki

Katika jamii nyingi za Kiafrika, bundi huonekana kama viumbe wa ajabu au alama za bahati mbaya. Baadhi ya watu huamini kuwa kuonekana kwa bundi juu ya paa ni ishara ya kifo au mkosi.

Wengine huamini kwamba sauti ya bundi ni wito wa roho, ambapo huamini washirikina wamekuja kwa njia ya ndege hao kuchukua uhai wa mtu. Soma hapa kufahamu zaidi kuhusu mila na imani potofu kuhusu bundi

Lakini hatari kubwa zaidi ni imani kuwa mayai ya bundi yana nguvu za kishirikina.

Biashara ya Mayai ya Bundi na Bundi Hai

Katika maeneo mbalimbali ya Tanzania, tumeweza kufanya mahojiano na watu waliowahi kushiriki au kushuhudia biashara ya mayai ya bundi.

Kwa mujibu wa maelezo yao, baadhi ya watu huamini kuwa mayai ya bundi yakitazamwa kupitia darubini yanaonesha michoro au alama maalum zinazofanana na umbo au mpangilio wa nyota, misikiti, au makanisa.

Umbo hilo huaminika kuwa na nguvu za kichawi au tambiko, na linaweza kutumika kuleta mafanikio ya biashara au utajiri.

Katika hali hii:

  • Mtu akikutwa na yai la bundi, huambiwa asiliguse kwa mkono wala mwili wake wote usigusane nalo.
  • Badala yake, yai hubebwa kwa kipande cha jani au nguo hadi kufikishwa kwa “mtaalamu” anayelichunguza.
  • Mayai haya huuzwa kwa bei kubwa sana, hadi kufikia maelfu ya shilingi kwa kila yai.

Wapo pia watu wanaonunua bundi akiwa hai kwa lengo la kufanya tambiko maalum, kwa imani kuwa bundi anaweza ‘kuamsha biashara’ au kuimarisha miradi yao ili “iishi usiku na mchana.”

Kwa mujibu wa makala ya “The criminal hunt for owl eggs in Kenya and Tanzania – A new sad poaching, between profits and beliefs” iliyoandikwa na Leni Frau mwaka 2024, biashara hii imehusishwa na mitandao ya uhalifu wa kimataifa, na inahusiana pia na imani za uponyaji wa magonjwa kama saratani na matatizo ya utotoni.

Bei ya mayai hayo imepanda hadi kufikia shilingi 100,000 kwa jozi (mayai mawili), na thamani yake kwa kilo inaweza kuzidi ile ya pembe ya kifaru au meno ya tembo.

Wanunuzi wakubwa wametajwa kuwa ni waganga wa kienyeji pamoja na wafanyabiashara toka mataifa ya Mashariki ya Kati.

Hali hii inaonyesha uhitaji wa haraka wa elimu ya jamii, uimarishaji wa sheria za uhifadhi, na kampeni za kubadili mitazamo kuhusu bundi kama viumbe wa mikosi.

Ukweli kuhusu michoro inayoonekana ndani ya mayai ya bundi kwa kutumia darubini

Michoro inayoonekana kwenye mayai ya bundi chini ya darubini ni matokeo ya muundo wa kibaolojia unaojulikana kama micropyle, ambayo ni sehemu ndogo inayoruhusu mbegu ya kiume kuingia na kurutubisha yai.

Aidha, mayai ya ndege huwa na matundu madogo sana (pores) yanazowezesha kubadilishana hewa, na yanaweza kuunda miale au mizunguko ya muundo wa mviringo unaoonekana kuwa wa kuvutia chini ya darubini.

Ingawa baadhi ya watu huona miundo hii kama inayofanana na nyota au nyumba za kuabudia, tafiti za kisayansi zinaonyesha kuwa hizi ni sifa za kawaida za kimaumbile katika mayai ya ndege, na hazina uhusiano wa moja kwa moja na alama za kidini au kiroho. Tafsiri hizo ni za kiimani na hazina msingi wa kisayansi.

Ukweli kuhusu Bundi kuhusishwa na Kifo

Katika jamii nyingi za Kiafrika, kumekuwa na imani potofu kwamba mlio wa bundi usiku ni ishara ya kifo kinachokaribia katika familia au nyumba fulani.

Wakati mwingine, hali ya mtu kufariki baada ya bundi kusikika akilia karibu na eneo hilo huchukuliwa kama uthibitisho wa imani hiyo.

Kuna nadharia isiyo na msingi wa kisayansi inayodai kuwa bundi ana uwezo wa kunusa seli za mwili zinazokufa, hivyo huanza kusogea karibu na eneo husika kwa matarajio ya kupata kitoweo endapo kiumbe hicho kitafariki.

Hata hivyo, utafiti wa kisayansi unaonyesha kuwa bundi hana uwezo mkubwa wa kunusa vitu vilivyo mbali.

Badala yake, ana uwezo wa kipekee wa kuona gizani na kusikia kwa usahihi mkubwa, ambao humsaidia kuwinda mawindo hai. Bundi si ndege anayekula mizoga, na ndiyo maana hawaonekani kwenye hospitali, mochwari, au maeneo yenye miili ya wafu.

Ukweli ni kwamba, baadhi ya wagonjwa walioko katika hali mbaya huweza kukata tamaa ya maisha wanaposikia mlio wa bundi, hasa pale ambapo imani za kijamii zinawafanya waamini kuwa mwisho wao umefika.

Hofu hiyo inaweza kuchangia kuzorota kwa hali ya mgonjwa, na wakati mwingine hata kifo. Lakini mara nyingi, tukio la kifo kufuata mlio wa bundi ni bahati isiyotarajiwa (coincidence) na si uhusiano wa moja kwa moja.

Imani hizi zimejengeka kwa karne nyingi, na zimechochewa zaidi na matumizi ya bundi na viumbe wengine kama njiwa, popo, na paka katika imani za jadi au kishirikina.

Hata hivyo, hofu kubwa imeelekezwa kwa bundi kutokana na sauti, sura yake ya kipekee na tabia yake ya usiku, hali inayohitaji kubadilishwa kupitia elimu na uhamasishaji wa jamii.

Athari za Imani hizi kwa Uhifadhi

  • Bundi wanawindwa, kukamatwa na kuuawa kinyume cha sheria.
  • Mayai yao huibwa kwenye viota kwa ajili ya biashara haramu, na kuathiri uzalianaji wao.
  • Makazi yao yanaathiriwa kwa kukata miti hovyo.
  • Hifadhi ya asili inapotea, na mnyororo wa chakula (food chain) unavurugika.

Kwa kuwa na imani potofu, jamii inaweka hatarini viumbe wanaosaidia kupunguza magonjwa (kwa kula panya, wadudu, nyoka n.k.), na kulinda kilimo chao.

Suluhisho Kupitia Uimarishaji wa Sheria, Elimu na Ushirikiano

Ingawa sheria za uhifadhi wa wanyamapori zipo nchini, utekelezaji wake kwa spishi zisizo maarufu kama bundi bado ni hautoshelezi hususani kwenye biashara haramu.

Sheria nyingi hulenga wanyama wakubwa kama tembo na vifaru, huku ukiukwaji wa haki za ndege wa porini ukiwa bado haujatiliwa maanani.

Ukosefu wa adhabu kali, pamoja na changamoto za ukosefu wa rasilimali kwa taasisi zinazohusika na uhifadhi, unachangia kuendelea kwa uhalifu huu.

Kuna haja ya kutunga sera mahsusi na kuimarisha utekelezaji wa sheria zinazolinda ndege wa porini, hasa wale walioko hatarini kama bundi, ili kuhifadhi urithi wa asili wa Afrika kwa vizazi vijavyo.

Mwandishi wa Makala hii pamoja na timu yake wanaendesha mradi wa utafiti na uhifadhi wa bundi na mazingira yao katika Milima ya Usambara Mashariki, na wamebaini kuwa taswira hasi katika jamii zinaweza kubadilika. Kupitia warsha, elimu za mazingira mashuleni, na video za elimu kwa lugha ya Kiswahili, wamefanikisha:

  • Kuongeza uelewa juu ya umuhimu wa bundi.
  • Kupunguza imani potofu na uoga wa usiokuwa na sababu.
  • Kuanza safari ya kurejesha mazingira na kuwa na jamii zinazoshiriki kikamilifu katika uhifadhi.

Kwa kushirikiana na makundi ya kijamii, serikali za vijiji, na mashirika ya ufadhili kama Rufford Small Grants, Conservation Leadership Programme, Raptors Aid, na Mohamed bin Zayed Species Conservation Fund, tumeanza safari ya kulinda viumbe hawa wa kipekee na kuhifadhi mazingira yao.

Hitimisho

Kupitia Makala hii fupi, tunapenda kubadili fikra na mitazamo ya kila msomaji wetu aliyekuwa na imani potofu juu ya bundi, na badala yake aanze kuwafurahia na kutamani kujifunza zaidi kuhusu maisha yao.

Bundi si ishara ya kifo ni viumbe wa kipekee wenye mchango mkubwa kwa mazingira yetu. Kupitia elimu na ushirikiano, tunaweza kubadili fikra potofu na kuhakikisha kwamba hata vizazi vijavyo vitawashuhudia viumbe hawa. Bonyeza hapa kusoma zaidi

Ni wajibu wetu sote kuwa walinzi wa viumbe hai na mali ya taifa letu.

Makala hii imeandikwa na Ezra Peter Mremi na kuhaririwa na Hillary Mrosso

Kwa maoni, ushauri au maswali unaweza kuwasiliana na mwandishi wa makala hii kwa mawasiliano yake hapo chini.

Ezra Peter Mremi
Mtaalamu wa Uhifadhi wa Wanyamapori | Mwanaharakati wa Mazingira | Mtafiti wa Bundi

Email: mremiezra@gmail.com

Phone: +255 756 438692

Tanzania

 

Kwa Nini Mikoko ni Muhimu Kuliko Miti ya Nchi Kavu?

0

Nukuu: “Mikoko ni hazina isiyothaminiwa, yenye uwezo wa kufyonza kaboni mara nne zaidi ya miti ya nchi kavu.”

Mazingira ya bahari yanahusisha maeneo yote yanayozunguka bahari ikijumuisha fukwe za bahari, misitu ya mikoko, majani bahari(seagrasses) na matumbawe.

Wengi hudhani kuwa mazingira ya bahari ni eneo tu la uso wa maji linaloonekana kwa macho huku wakisahau hayo maeneo mengine muhimu.

Mandhari safi ya bahari hususani maeneo ya fukwe hutumiwa sana na watalii wa ndani na nje nchi kupumzika na kufurahia upepo mwanana unaosindikizwa na sauti za mawimbi ya maji kutoka baharini.

Watu wengi wanaobahatika kutembelea maeneo haya huweza kupata nafasi ya kuona viumbe wengi wa baharini wakitambaa katika fukwe hizo mfano kasa, konokono,yavuyavu, samaki nyota n.k.

Licha ya umuhimu huo bado utunzaji wa mazingira mengine ya bahari umesahaulika na hata juhudi zinazochukuliwa kutunza maeneo haya bado hazitoshelezi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Raisi Muungano na Mazingira, Mh. Dr. Selemani Jafo akishiriki kupanda miti aina ya mikoko.

Licha ya maeneo haya kuwa na umuhimu mkubwa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kama vile uwezo mkubwa wa kufyonza hewa ukaa au hewa ya kaboni.

Mabadiliko ya tabianchi yanayoshuhudiwa katika kona mbalimbali za dunia yamekuwa yakichangiwa na mkusanyiko wa hewa ukaa angani jambo linaloathiri ustawi wa dunia kimazingira hivyo kuathiri pia sekta nyeti hasa za kilimo na ufugaji.

Hewa ukaa imekuwa ikizalishwa kwa wingi duniani kutokana na maendeleo katika sekta ya viwanda,usafirishaji,uchimabaji madini na kilimo. Makala inayoelezea biashara ya hewa ukaa kwa ujumla, unaweza kuisoma hapa

Hivyo basi, mazingira ya bahari yanamchango mkubwa katika kupunguza hewa ukaa na kuiweka dunia katika hali nzuri.

Elimu ya utunzaji wa mazingira ya bahari imekuwa ikitolewa kwa uchache, ikiwa ni pamoja na miradi ya kaboni ukilinganisha na elimu ya utunzaji wa uoto wa nchi kavu; hivyo watu wengi hawana elimu ya kutosha juu ya uhusiano uliopo kati ya hewa ukaa na mazingira ya bahari.

Picha ya msitu wa mikoko, picha kutoka mtandaoni.

Kipi kinapunguza hewa ukaa Kwa kiasi kikubwa kati ya Mazingira ya bahari na mimea ya nchi kavu?

Hili ni swali muhimu ambalo majibu yake yanaleta changamoto kwa watu wengi. Miradi mingi ya kaboni inayolenga kupunguza hewa ukaa katika kanda za bahari ni michache.

Tunaona nguvu kubwa ikielekezwa katika uoto wa nchi kavu, jambo ambalo limepelekea watu kuamini kuwa pengine uoto wa asili unaopatikana nchi kavu ndio mwarobaini wa kufyonza kiasi kikubwa cha hewa ukaa.

Ukweli ni kwamba mazingira ya bahari yanauwezo wa kupunguza kiasi kikubwa cha hewa ukaa mara nne zaidi, ukilinganisha na kiasi cha hewa ukaa ambacho kinaweza kufyonzwa na uoto wa mimea ya nchi kavu.

Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine wakiwa katika mafunzo ya vitendo katika mazingira ya bahari yenye misitu ya mikoko, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Picha na Victor Wilson

Hii inaonyesha wazi kuwa mazingira ya bahari ni miongoni mwa tunu pekee zilizobaki zenye uwezo mkubwa wa kuinusuru dunia dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

Tafiti zinaonyesha kuwa kiasi cha hewa ukaa kinachofyonzwa na misitu ya mikoko ni kikubwa zaidi kuliko miti ya kawaida.

Lakini pia udongo unaopatikana katika misitu ya Mikoko inauwezo mkubwa wa kutunza kiasi kikubwa cha hewa ukaa(Soil-carbon sequestration);

Hii ni kutokana na asili ya udongo huu kushikamana sana na kutengeneza tope zito ambalo haliwezi kuruhusu tena kaboni/hewa ukaa iliyohifadhiwa kurudi angani.

Lakini pia, uozo wa asili unaopatikana Baharini husaidia kutunza kiasi kikubwa cha hewa ukaa, kama alivyoandika mwandishi Benner na wenzake mwaka 1984.

Mazingira ya nchi kavu na bahari yameleta taswira mtambuka kiuchumi hasa kwa kuhusianisha rangi ya kijani na bluu.

Uchumi wa bluu umechukua dhana hii ikimaanisha uchumi unaotokana na rasilimali zitokanazo na bahari. Soma hapa kufahamu zaidi

Aina hii ya uchumi inahusisha shughuli mbalimbali kama uvuvi, utalii, ufugaji wa samaki na usafiri. Shughuli zote hizo zinafanyika kwa misingi ya uhifadhi wa ikolojia ya bahari pamoja na mazingira yake.

Falsafa ya uchumi wa bluu imesaidia Kwa kiasi kikubwa kuhifadhi mazingira ya bahari na kuinua watu kiuchumi huku wakiacha mazingira ya bahari yakiwa salama.

Kutoka kushoto ni mwandishi wa makala hii Victor Wilslon, Prof. RPC Temu, Mhadhiri Chuo Kikuu Cha Sokoine Cha kilimo,  na Mtaalamu wa Sayansi ya misitu wakiwa katika misitu ya mikoko Hifadhi ya Taifa ya Saadani.

Je? Unajua maana ya kaboni ya kijani na kaboni ya bluu??

Kutokana na muktadha wa nchi kavu na Bahari zimesababisha uwepo wa aina mbili za kaboni/hewa ukaa ambazo ni kaboni ya kijani na kaboni ya bluu.

Licha ya hayo, rangi ya kijani na bluu hazimaanishi rangi halisi za viwango vya kaboni vinavyopatikana katika maeneo hayo.

Kaboni ya kijani ni aina ya kaboni ambayo mchanganuo wake uko kama ifuatavyo;

  • Hii ni aina ya kaboni ambayo inafyonzwa na mimea ya nchi kavu ikihusisha misitu, nyasi na kilimo. Misitu hufyonza kaboni inayopatikana angani kupitia majani yake.Rangi ya kijani ya uoto wa misitu na majani umesababisha kaboni inayopatikana katika maeneo hata kupewa rangi ya kijani.
  • Kaboni ya kijani huhifadhiwa katika miti, mizizi,na udongo. Sehemu hizo hufanya kazi ya kutunza gesi ya kaboni inayofyonzwa na majani kupitia usanisi nuru. Udongo imara huweza kutunza kiasi kikubwa cha kaboni na ukubwa wa mti huweza kubainisha kiasi cha kaboni iliyohifadhiwa. Uhai na uwepo wa misitu mikubwa huashiria wingi wa kaboni unaoweza kuhifadhiwa.

Lakini pia, kaboni ya bluu ni aina ya pili ya kaboni ambayo inaelezewa na mchanganuo ufuatao;

  • Kaboni ya bluu hutokana na gesi ya kaboni inayofyonzwa kutokana na mimea ya pwani na Baharini. Miti ya mikoko, majani bahari, matumbawe n.k huhifadhi kaboni inayobeba rangi ya bluu.
  • Uimara wa misitu ya mikoko na aina ya udongo,kupwa na kujaa kwa maji katika mazingira ya bahari hufanya mazingira haya kuwa kinara katika kuhifadhi viwango vikubwa vya kaboni ukilinganisha na uoto wa nchi kavu.
  • Licha ya kuhifadhi viwango vikubwa vya kaboni pia huhifadhi bayoanuai muhimu ambazo zisipohifadhiwa zinaweza kutoweka hasa jamii ya amfibia, Reptilia n.k. Wanasayansi na watafiti wamejaribu kutumia rangi ya vitu halisi katika kuwasilisha matokeo ya tafiti zao kiurahisi.
  • Mwandishi Nellemann (2009), aliapendekeza kutumia jina la kaboni ya bluu litumike kuwakilisha kaboni inayopatikana katika maeneo ya bahari kutokana na kuwa tafiti zake zilijikita katika maeneo hayo.

Kwa dhana hiyo Mazingira ya bahari yanamchango mkubwa katika kukabiliana na madhara yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi.

Utafiti uliofanywa na Mpango wa Ikweta kupitia Shirika la Mikoko la nchini Kenya lilibainisha kuwa mikoko inayopatikana pwani ya Kitropiki na chini ya Kitropiki inakabiliwa na changamoto mbalimbali.

Kuna nchi 15 duniani zenye zaidi ya 75% ya misitu ya mikoko. Nchi hizo zinakabiliwa na changamoto ambazo zinatishia uhai wa muda mrefu wa misitu hii duniani.

Nchi kama Indonesia, Brazil, Nigeria na Mexico huchukua zaidi ya 40% ya mikoko duniani zenye hekta milioni 6.5.

Nchi nyingine zenye utajiri wa mikoko ni India, Malaysia, Australia na nchi za kusini mashariki mwa bara la Asia ambazo ni Thailand, Vietnam, Myanmar na ufilipino.

Na tafiti hiyo ilibainisha kuwa kuna 7% ya misitu ya mikoko ambayo imehifadhiwa. Hii inaonesha ni jinsi gani ambavyo kuna pengo kubwa katika uhifadhi wa mikoko licha ya ubora wake katika soko la hewa ukaa.

Tanzania, Madagascar na Msumbiji ni miongoni mwa nchi zinazopatikana katika bara la Afrika zenye utajiri wa Mikoko.

Misitu hii ya ukanda wa bahari imekuwa ni hazina kubwa kutokana na umuhimu wake mkubwa katika kufyonza hewa ukaa, lakini pia bado inamchango mkubwa kiuchumi,ki-ikolojia, kisayansi na kijamii.

Jamii Rufiji, ikishiriki katika kupanda miti aina ya mikoko katik, picha na Kizito Makoye

Matumizi ya nishati ya kuni inayotokana na miti ya mikoko, upasuaji wa mbao, uanzishwaji wa miundombinu mbalimbali ya ujenzi ni vitendo ambavyo vinaathiri ustawi wa misitu hii.

Mazingira ya bahari husaidia kukuza uchumi wa nchi kutokana na uwezo wake wa kutunza mazalia ya samaki.

Samaki huzaliana kwa wingi katika maeneo tulivu hasa maeneo ya mikoko ambayo haiathiriwi na mawimbi makali ya bahari na kuweka ikolojia ya bahari katika ustawi wake.

Sekta ya uvuvi imekuwa na mchango mkubwa kiuchumi katika nchi mbalimbali duniani hivyo kukuza pato la taifa, mfano nchi ya Norway huweza kukusanya zaidi ya Trilioni 40 kutokana na makusanyo katika sekta ya uvuvi.

Licha ya hayo, maeneo ya bahari ni makazi ya Ndege na viumbe wengine ambao  huweza kuweka viota vyao na kuendeleza maisha Yao katika misitu hii.

Napenda kutoa rai kwa serikali, sekta binafsi na wananchi kuzidi kuweka mkazo juu ya uhifadhi wa mazingira ya bahari, ili kuweza kufikia misingi mizuri ya uchumi wa bluu na mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

Mchango wako msomaji ni muhimu sana katika kujenga uchumi na uhifadhi endelevu, kutoa elimu juu ya matumizi sahihi ya bahari na rasilimali zake.

Makala hii imeandaliwa na Mhifadhi, Victor Wilson na kuhaririwa na Hillary Mrosso. Kama utakuwa na maswali, maoni, ushauri usisite kuwasiliana na mwandishi wa makala hii kwa mawasiliano hapo chini.

Victor Wilson

Barua pepe: wilsonvictor712@gmail.com

Simu: +255620861002

Whatsapp: +255743880175

Usiyoyajua Kuhusu Kwezi Maridadi na Umuhimu Wake Katika Ikolojia

1

Kwezi Maridadi au Kuzi ni ndege wa kuvutia kutoka familia ya Musophagidae, anayejulikana kwa manyoya yake ya rangi ang’avu kama bluu-kijani, nyeusi, nyeupe na nyekundu kahawia.

Anapatikana maeneo ya uoto wa wazi sehemu kame, nyasi na miti michache, mashambani, mijini na kwenye bustani.

Hupatikana nchini Tanzania, Kenya, Uganda, Ethiopia, Somalia na Sudani kusini barani Afrika pekee.

Picha ya Kwezi Maridadi, Chanzo cha picha: superb¬¬- wikiwand articles

Licha ya uzuri wake, spishi hii inakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazotishia uwepo wake, ikiwa ni pamoja na uharibifu wa makazi na uwindaji haramu.

Makala hii itaelezea kwa kina biolojia ya Kwezi Maridadi, umuhimu wake katika mfumo wa ikolojia, na hatua zinazoweza kuchukuliwa ili kuhifadhi ndege huyu adimu

Kwezi Maridadi ni ndege wa ukubwa wa wastani, akifikia urefu wa takribani semtimita18-19, na uzito wa gramu 50-75.

Ana sifa zifuatazo za kipekee

Manyoya yenye rangi angavu, yanayosaidia katika mchakato wa mawasiliano na kujificha dhidi ya wanyama wanaowinda.

Mkia wenye rangi ya kuvutia, unaotumika kusaidia usawa wakati wa kuruka.

Miguu yenye vidole vinavyoweza kushikana kwa nguvu, inayomwezesha kupanda miti kwa urahisi.

Lishe yake inajumuisha matunda, mbegu na wadudu, hivyo kuwa na jukumu muhimu katika mzunguko wa chakula na kusambaza mbegu katika ikolojia yake.

Hutaga mayai 2-6 meupe au bluu katika tundu la mti, na mayai hayo hutagwa kwa mzunguko wa miezi michache kila mwaka.

Picha ya Kwezi Maridadi, Picha na Sukuro Etale kutoka Facebook

Umuhimu wa Kwezi Maridadi Katika Mfumo wa Ikolojia

Kwezi Maridadi ana nafasi muhimu katika mfumo wa Ikolojia, na mchango wake unajumuisha yafuatayo:

  1. Usambazaji wa mbegu – Anapokula matunda, kwezi maridadi humeza mbegu na kuzisambaza kupitia kinyesi chake. Hii husaidia katika upandaji wa miti na urejeshaji wa uoto.
  2. Udhibiti wa wadudu – Kwa kula wadudu kama vile viwavi na nzige husaidia kupunguza idadi ya wadudu waharibifu wa mimea.
  3. Kudumisha uwiano wa mazingira – Kama sehemu ya mnyororo wa chakula, kwezi maridadi huchangia katika uwiano wa viumbe hai.
  4. Kuvutia watalii – Urembo wa ndege huyu huwavutia watalii wanaokuja kushuhudia aina mbalimbali za ndege wa Kiafrika, hivyo kusaidia kuinua uchumi wa maeneo husika.

Changamoto Zinazotishia Uhai wa Kwezi Maridadi

Pamoja na umuhimu wake mkubwa katika mfumo wa ikolojia, Kwezi Maridadi anakabiliwa na changamoto kadhaa zinazotishia uhai wake. Baadhi ya changamoto hizo ni:

  1. Uharibifu wa makazi yake – Ukataji wa miti na upanuzi wa shughuli za binadamu, kama kilimo na ujenzi wa makazi, unasababisha kupungua kwa maeneo salama ya kwezi maridadi kuishi na kutaga mayai.
  2. Uwindaji na biashara haramu – Kutokana na rangi nzuri ya manyoya yake, kwezi maridadi hunaswa na kuuzwa kama mnyama wa mapambo au hutumiwa kwa imani za kijadi.
  3. Mabadiliko ya tabianchi – Mabadiliko haya huathiri upatikanaji wa chakula na maeneo salama ya kutaga kwa kwezi maridadi, hivyo kupunguza idadi yao kwa kasi.
  4. Mashambulizi ya wanyama wakali – Ndege huyu pia anakumbwa na tishio la kuliwa na wanyama kama mwewe, nyoka, na paka mwitu, hasa vifaranga na mayai yake.

Mbinu za Kuhifadhi Kwezi Maridadi

Ili kuhakikisha kwamba Kwezi Maridadi anaendelea kuishi na kustawi, hatua zifuatazo zinapaswa kuchukuliwa:

  1. Kulinda na kuhifadhi mazingira yake; Serikali na mashirika ya uhifadhi yanapaswa kuongeza jitihada za kusimamia utuzwaji wa uoto na mazingira asilia.
  1. Kuzuia uwindaji na biashara haramu; Sheria kali zinapaswa kuwekwa ili kupiga marufuku uwindaji na biashara ya kwezi maridadi kama mnyama wa mapambo.Vikundi vya jamii vinaweza kusaidia kwa kuripoti wawindaji haramu kwa mamlaka husika.
  1. Kuanzisha maeneo ya hifadhi; Hifadhi za ndege na mbuga za wanyama zinaweza kusaidia kulinda makazi ya kwezi maridadi. Programu za upandaji miti ya asili zinapaswa kuimarishwa ili kurejesha mazingira ya asili ya ndege hawa.
  1. Elimu na uhamasishaji kwa jamii; Kampeni za elimu zinaweza kufanyika ili kuwafahamisha wananchi kuhusu umuhimu wa kwezi maridadi na mchango wake katika ikolojia. Shule na vyombo vya habari vinaweza kutumika kama njia za kueneza elimu ya uhifadhi wa ndege na viumbe hai.
  1. Tafiti na ufuatiliaji wa idadi ya Kwezi Maridadi; Tafiti zaidi zinapaswa kufanyika ili kubaini mabadiliko katika idadi na mwenendo wa kwezi maridadi na hali ya makazi yao. Matokeo ya tafiti hizi yanaweza kusaidia kutengeneza sera bora za uhifadhi.

Pichani ni Kwezi Maridadi, picha na  Sukuro Etale, kutoka katika mtandao wa Facebook

Hitimisho

Kwezi maridadi ni ndege mwenye thamani kubwa katika mfumo wa ikolojia na utalii wa mazingira.

Hata hivyo, changamoto kama uharibifu wa makazi, uwindaji haramu, na mabadiliko ya tabianchi zinaendelea kutishia uwepo wake.

Ili kuhakikisha kuwa kizazi kijacho kinaweza kumshuhudia ndege huyu wa kipekee, ni muhimu kuchukua hatua za uhifadhi kwa kushirikiana kati ya jamii, serikali, na mashirika ya uhifadhi.

Kwa pamoja, tunaweza kuokoa kwezi maridadi na kuhifadhi urithi wa asili kwa vizazi vijavyo.

Makala hii imehaririwa na Ester Matingisa, ambaye ni mtalaamu wa ndege kutoka Tanzania

Kwa maswali, maoni, ushauri, mapendekezo, usisite kuwasiliana na mwandishi wa makala hii kwa mawasiliano hapo chini;

Daud Jacob Kanyamaha

0746423034

Kanyamaha.dj@gmail.com

 

 

Tunaandika makala hizi ili tuongeze uelewa wetu kuhusu wanyamapori, tunaamini tukipata uelewa tutachukua hatua kushiriki katika uhifadhi wa wanyamapori na mazingira yake asilia.Kazi hii tunafanya kwa kujitolea na hakuna malipo yoyote, endapo umefurahia kazi zetu unaweza kutuunga mkono kwa kiasi chochote ili tupate mtandao, vifaa vyua kufanyia kazi kama kamera na komputa. Kwa maelezo zaidi unaweza kuwasiliana kwa mawasiliano haya; hmconserve@gmail.com  |+255-683-862-481

Sababu za Hifadhi ya Taifa ya Serengeti Kushinda Tuzo ya Hifadhi Bora Barani Afrika

0

Hifadhi yetu ya Taifa ya Serengeti imekuwa ikituwakilisha vyema kiukanda, barani Afrika na duniani kwa ujumla kupitia tuzo hii ya hifadhi bora barani Afrika inayoandaliwa na shirika binafsi, World Travel Awards.

Serengeti imekuwa ikishinda tuzo hii adhimu kwa miaka saba sasa mfululizo, 2019 – 2025.

Shirika hili la World Travel Awards lenye makao makuu mjini London – Uingereza, limekuwa likijihusisha katika uandaaji na ugawaji wa tuzo mbalimbali katika sekta ya utalii, usafiri, hotelia na huduma kwa wageni.

Tuzo hizi zimekuwa kama sehemu ya kutambua na kupongeza ubora na juhudi kubwa za uhifadhi wa hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Wawakilishi wa Tanzania waliopokea tuzo ya hifadhi bora barani Afrika, hifadhi ya taifa ya Serengeti 2024; picha na World Travel Awards

Tuzo hii ilianzishwa mwaka 2013 ikiwa na wawaniaji sita, ambao ni;

  • Hifadhi ya taifa ya Serengeti – Tanzania,
  • Maasai Mara – Kenya,
  • Etosha – Namibia,
  • Kidepo – Uganda,
  • Kruger – Afrika kusini na
  • Central Kalahari nchini Botswana.

Wawaniaji hawa idadi yao imekuwa hivyo kwa miaka yote isipokuwa mwaka huu 2025, Maasai Mara – Kenya imejitoa katika orodha.

Hifadhi hizi zimekuwa zinafuata taratibu za usajili na uandikishaji, kisha kufuatiwa na upigaji kura wa wazi wenye kuruhusu watu wote kupiga kura. Baada ya hapo, shirika hufanya mchujo na mwishowe kutangaza mshindi.

Mshindi wa kwanza wa tuzo hii kwa miaka sita mfululizo ni hifadhi ya Maasai Mara nchini Kenya, (2013 – 2018) kisha kupokelewa na hifadhi yetu ya taifa ya Serengeti kwa miaka saba mfululizo, 2019 – 2025.

Tuzo ya mwaka 2025 iliyotolewa jijini Dar es salaam – Tanzania, tarehe 28 Juni.

Tuzo hii ya hifadhi bora barani Afrika, ni miongoni mwa tuzo kubwa sana za kikanda barani Afrika, ikifuatiwa tuzo ya Kivutio bora cha utalii barani Afrika na Eneo Bora la Safari Duniani.

Ukubwa wa tuzo hizi umesababishwa na chachu yake katika kutangaza vivutio vyetu vya utalii na kuvutia uwekezaji wenye tija.

Hifadhi zinazowania tuzo hii, ni hifadhi bora barani Afrika na duniani kwa ujumla zenye vigezo vifwatavyo; –

Uzoefu wa mgeni; hapa kuna mambo mengi sana ambayo yanategemea juhudu jumuishi za hifadhi, wawekezaji na wamiliki wa kampuni za utalii, hoteli na kambi.

Mandhari nzuri ya miundombinu ya nyumba za wageni, zikiwa zimejengwa kuzingatia mazingira asilia kabisa; Picha kutoka Serengeti National Park, https://www.serengetiparktanzania.

Juhudi hizi kwa pamoja zina nafasi kubwa ya kumfanya mgeni afurahie safari yake hivyo kuitangaza hifadhi kwa ukubwa na hata kupiga kura kwa urahisi.

Juhudu hizi huanzia kwenye ubora wa miundombinu ya hifadhi husika kama vile barabara, mitandao, viwango vya ubora wa hoteli na kambi, huduma zinazotolewa pamoja na watoaji huduma, upatikanaji wa habari sahihi, ulinzi na usalama wa hifadhi husika na nchi kwa ujumla pia aina mbalimbali za shughuli anazoweza kuzifanya.

Vile mgeni anavyojisikia kuanzia kupokelewa, atakavyohudumiwa hotelini/ kambini ile miingiliano na wafanyakazi, pia upatikanaji wa taarifa wa wazi na sahihi husaidia kumridhisha mgeni na hivyo kuongeza nafasi kubwa sana ya kuwania tuzo hii.

Athari za uhifadhi; kigezo hiki huangaza katika athari chanya za uhifadhi. Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, kupitia shirika la hifadhi za Taifa TANAPA, imewekeza juhudi nyingi katika uhifadhi endelevu wenye matokeo chanya kama vile ongezeko la idadi ya wanyama ndani ya mifumo ya ikolojia.

Juhudi hizo ni pamoja na ufanyaji doria usiku na,mchana, angani na nchi kavu kuhakikisha usalama na utulivu wa binadamu na wanyama.

Pia sheria zenye kuonya na kuzuia uendeshaji mbaya wa magari hifadhini zimewezesha hifadhi ya Serengeti kushuhudia ongezeko kubwa la wanyama kama nyati na tembo.

Kupungua kwa changamoto za ujangili umechangia wanyama kuongezeka na kuifanya hifadhi ya Serengeti kuwa na mvuto na mandhari nzuri .

Uhifadhi chanya pia unahusisha kusaidia jamii za pembezoni mwa hifadhi katika kubuni na kuanzisha miradi ya kiuchumi kwa mfano utengenezaji na uuzaji wa shanga, picha za wanyama, vikoi na shuka za kimasai. Juhudi zote hizi huchangia kuwezesha shughuli za utalii ndani ya hifadhi.

Bayoanuai ya viumbe na mifumo ya ikolojia ndani ya hifadhi; Viumbe hai kama vile ndege, wanyama, wadudu na mimea ndani ya mifumo ya kiikolojia huwezesha mlinganyo wenye kuleta usawazishi baina yao.

Ndani ya hifadhi tunaona viumbe mbalimbali wakubwa kwa wadogo wenye kupeperusha vyema bendera ya Serengeti kwa mfano nyumbu, pundamilia, jamii mbalimbali za swala.

Pia Seregeti ni miongoni mwa hifadhi zinazotunza spishi zilizoko hatarini kutoweka katika uso wa nchi kwa mfano faru weusi, mbwa mwitu na jamii nyingi za tumbusi.

Bayoanuai hizi zote huchangia sana katika kumfanya mgeni kuifurahia safari yake hivyo huzingatiwa zaidi katika mchuano wa tuzo hii.

Utalii endelevu; aina hii ya utalii huhimiza zaidi kupunguza uzalishaji wa uchafu pia unagusa maisha ya jamii jirani kupititia ajira na uchangiaji wa mifuko ya maendeleo ya jamii.

Mandhari nzuri na yenye mvuto ya Hifadhi ya Taifa; Picha na Kjekol

Aina hii ya utalii hulenga wamiliki na wawekezaji wa utalii katika matumizi bora ya vifaa, mifumo na sheria wezeshi za utunzaji taka pia huhimiza utumiaji wa nishati bora kama ya jua.

Kambi na hoteli nyingi ndani ya hifadhi ya Serengeti hutumia nishati ya umeme wa jua kuendesha shughuli zao mfano kuchaji ‘golf car’ kwa matumizi madogo ndani ya kambi.

Baadhi ya kampuni gari zao zimekuwa zikitumia nishati hii ya umeme wa jua kuendeshea gari za watalii kama vile Miracle experience, hivyo kupunguza uchafuzi wa hali ya hewa.

Utalii huu endelevu pia umekuwa msaada katika kutunza na kuheshimu tamaduni za wazawa kama vile Wamaasai kuishi kwenye boma zao na Wahadzabe kuishi msituni. Zaidi soma makala hii Fahamu Vichochezi Tisa (9) vya Kusaidia Kutangaza na Kukuza Utalii Duniani

Mashirika mbalimbali duniani yamekuwa yakijitokeza kusisitiza aina hii ya utalii ili kutunza na kusimamia usalama kwa binadamu na wanyama.

Uzuri wa asili wa hifadhi; uzuri huu huzingatiwa kwenye uasilia wa eneo husika pamoja na viumbe wake, mimea mbalimbali, aina za uoto na jiographia nzima kama vile milima, miinuko na tambarare za nyasi.

Makundi ya Nyumbu yakiwa yanavuka mto Mara katika hifadhi ya taifa ya Serengeti. Picha na Janie Nikola

Hifadhi ya Serengeti ina uzuri wa asili mkubwa kuanza na aina za wanyama wengi wenye kuvutia ndani ya tambarare kubwa ya nyasi fupi.

Pia hifadhi yetu imepabwa kwa mawe makubwa na miamba inayochangia uzuri wake, ikijaziwa na uoto wa aina tofauti tofauti wenye kusaidia ukuaji na muingiliano mzuri wa wanyama ndani ya hifadhi.

Tuzo hizi zina mchango mkubwa sana katika sekta ya utalii hasa kwenye kutangaza na kukuza jina la nchi na hifadhi husika.

Tuzo hizi zimekuwa chachu katika kuhamasisha juhudu za nchi kwenye kuendeleza na kutunza vivutio vyetu.

Na hivyo kufananishwa na tuzo za Oscar ambazo ndizo tuzo kubwa sana duniani katika uwanja wa filamu.

Kwa nafasi hii mpendwa msomaji naamini utakuwa balozi mzuri wa kuhamasisha upigaji kura, utunzaji mazingira na kudumisha utalii endelevu.

Kwa maoni na ushauri usisite kuwasiliana na mwandishi wa makala hii kwa mawasiliano hapo chini

 Leena Lulandala – +255 755 369 684|| leenalulandala0@gmail.com

 

Tunaandika makala hizi ili tuongeze uelewa wetu kuhusu wanyamapori, tunaamini tukipata uelewa tutachukua hatua kushiriki katika uhifadhi wa wanyamapori na mazingira yake asilia.Kazi hii tunafanya kwa kujitolea na hakuna malipo yoyote, endapo umefurahia kazi zetu unaweza kutuunga mkono kwa kiasi chochote ili tupate mtandao, vifaa vyua kufanyia kazi kama kamera na komputa. Kwa maelezo zaidi unaweza kuwasiliana kwa mawasiliano haya; hmconserve@gmail.com  |+255-683-862-481