More

    SHAIRI: Tutunze Makazi ya Simba

    Picha imepigwa na Hillary Mrosso, katika hifadhi ya Taifa ya Nyerere, Tanzania

    1.Ndugu zangu karibuni, nina jambo kutamka
    Simba wapo hatarini, majangili wawasaka
    Waharibu masikani, kuvuka yao mipaka
    Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

    2.Simba waisha porini, hali sipobadilika
    Hatua tuchukueni, tusije tukaumbuka
    Wabaya tuwajueni, ikibidi kuwashika
    Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

    3.Mikakati tuwekeni, ujangili tumechoka
    Mizaha tweke pembeni, na tuingiwe mashaka
    Sijekuwa masikini, uchumi wetu kushuka
    Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

    4.Zaja hela za kigeni, Utalii kifanyika
    Tutafuta na madeni, nchi itaheshimika
    Tutatamba duniani, washindi tutaibuka
    Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

    5.Simba haba hifadhini, malaki hawajafika
    Waweza usiamini, lakini waongezeka
    Siweke silaha chini, bado hatujaridhika
    Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

    6.Kalamu naweka chini, nimechoka kuishika
    Nimefikia mwishoni, wa shairi kuandika
    Wekeni haya moyoni, daima kuyakumbuka
    Simba wanayo thamani, tutunze makazi yao

    Hillary Mrosso| mrossotm@gmail.com
    +255 683 862 481 |Morogoro| 10.08.2025

    Latest articles

    Related articles

    Leave a reply

    Please enter your comment!
    Please enter your name here