More

    Shairi: “Bundi ndege wa pekee ( U-1)

    Karibu kwenye shairi linalohamasisha uhifadhi wa ndege aina ya Bundi. Shairi hili limendikwa na Dr. Raymondi Mgeni, maarufu kama Malenga wa Ubena, unaweza kusoma na kuwashirikisha wengine. Karibu!

    Bundi aina ya Spotted-Eagle, anapatikana katika milima ya Usambara. Picha na Ezra Mremi

    Zipo imani potofu, zimwandamazo bundi
    Jamii hujawa hofu, navyo vitu haviendi
    Bundi si mharibifu, kwanini hatumpendi ?
    Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

    Jamii imeamini, bundi kabeba mikosi
    Wakimuona nyumbani, wanajawa wasiwasi
    Wasema leo kunani, wataja hii nuksi
    Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

    Tena bundi akilia, hawazizimi taa
    Hofu inawaingia, kuwa sasa ni balaa
    Wanajua lawajia, tetesi zitazagaa
    Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

    Kahusishwa na uganga, na haramu biashara
    Nia ovu wanapanga, bundi apate madhara
    Avamiwa na mapanga, eti anatisha sura
    Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

    Bundi anazo faida, na nyingi za ikolojia
    Si wa alama ya shida, wa kuleta mbaya njia
    Ni ndege wa kawaida, na vingi husaidia
    Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

    Twaona zipo dalili, ndege kutupokonyoka
    Spishi zake mbalimbali, kuja kesho kutoweka
    Hili tulione mbali, na jamii ikazinduka
    Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo

    Tutoe hii elimu, jamii na kila kona
    Ni biashara haramu, bundi kutafutwa sana
    Uwepo wake muhimu, nayo kubwa tu maana
    Bundi ndege wa pekee, na si vile tujuavyo.

    Picha ya Bundi, imepigwa na Ezra Mremi

    Malenga wa Ubena
    +255 676 559 211
    raymondpoet@gmail.com
    Uhifadhi wa Bundi
    Wildlife Tanzania

    Latest articles

    Related articles

    Leave a reply

    Please enter your comment!
    Please enter your name here